• Unataka Kujenga Ukuta Imara wa Nyumba Yako Utakaodumu Muda Mrefu?

    Ukuta wa nyumba ni sehemu muhimu na ya kudumu katika jengo lolote. Huweka uimara wa jengo na kudhibiti joto la nje na la ndani sambamba na kuweka usiri wa vitu vilivyomo ndani ya jingo. Hutoa ulinzi na kuweka usalma dhidi ya matukio ya hatari na wizi kwa vitu ama watu waliomo ndani.

  • Tunakosa nini Tusipotumia Wataalamu katika Ujenzi Wetu?

    Kushirikisha wataalamu kunatoa fursa ya kujua mbinu mpya na bora za ujenzi, kufaahamu vifaa vya ujenzi na sifa zake, kujua namna ya kupata gharama nafuu za ujenzi na usanifu majengo kuendana na ndoto yako binafsi.

  • Unafahamu Nini Ukinunua Simenti Imeandikwa 32.5N au 42.5N?

    Kuna madaraja matatu ya ubora/uimara wa simenti/saruji ambayo ni uimara wa chini 32.5, uimara bora zaidi ya ule wa chini 42.5 na uimara wa juu zaidi 52.5. Saruji ya gredi 52.5 bado haijaanza kuzalishwa kwa soko la Tanzania. Hii ni kusema kwamba tuna gredi ya 32.5 na 42.5 tu.Simenti ya daraja la chini la ubora 32.5 inafaa zaidi kwa matumizi ya plaster na kazi ndogo ndogo, na ile ya daraja la juu zaidi yani 42.5 inafaa zaidi kwa kazi za zege kama nguzo, bimu, slabu, madaraja n.k kutokana na uimara wake kuwa mkubwa zaidi.

Friday, December 22, 2017

Huyu Ndiye Wakala wa Taifa wa Utafiti wa Nyumba Bora na Vifaa vya Ujenzi !? Soma hapa kufahamu kazi zao.

Mabweni ya wasichana kwenye Shule ya Sekondari Mubaba Wilayani Biharamulo yaliyojengwa kwa kutumia matofali ya kufungamana ikiwa ni sehemu ya usambazaji wa teknolojia hiyo. PICHA NA NHBRA
Tanzania kama zilivyo nchi nyingine zinazoendelea imekuwa ikikabiliwa na upungufu wa nyumba bora. Kwa miongo mingi Serikali zote kabla na baada ya uhuru zilitambua matatizo ya nyumba, umuhimu na uharaka wa kuyatatua.

Juhudi mbalimbali zimefanywa kushughulikia tatizo hilo. Ilifikiriwa kwamba ufumbuzi wa kudumu wa tatizo hili ni kuunda taasisi zitakazokuwa na wajibu wa kutoa mafunzo katika sekta ya nyumba ili kuboresha na kuongeza msingi wa ubora wa nyumba kutokana na tatizo kuendelea kuwapo. Serikali iliamua kuunda upya kituo cha Utafiti wa Ujenzi (BRU), kuwa Wakala wa Taifa wa Utafiti wa Nyumba Bora na Vifaa vya Ujenzi (NHBRA), yenye mamlaka ya kuendesha shughuli kibiashara.

Wakala wa Taifa wa Utafiti wa Nyumba Bora na Vifaa vya Ujenzi umejikita katika kufanya utafiti katika maeneo yafuatayo:- Mbinu za ujenzi, Vifaa vya ujenzi, Gharama za ujenzi na usanifu majengo na Uchumi na kijamii.

Wakala wa Taifa wa Utafiti wa Nyumba Bora na Vifaa vya Ujenzi ni Wakala ya Serikali iliyoanzishwa tarehe 1 septemba 2001. Wakala hii iko chini ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Ofisi zake ziko Mwenge barabara ya Sam Nujoma Wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam, umbali wa mita 400 kutoka barabara ya Ali Hassan Mwinyi.

KAZI ZA NHBRA
Kufanya utafiti kuhusu nyenzo za ujenzi na teknolojia ya ujenzi katika ngazi ya matumizi
Kushirikiana na Mamlaka za Serikali Kuu na Serikali za Mitaa, Asasi zisizo za Kiserikali, Mashirika ya Kijamii, Wabia wa maendeleo na watu binafsi katika kuunda na kutoa mafunzo kwa /vikosi vya ujenzi wa nyumba na uzalishaj vyenzo katika ngazi ya wananchi.
Kuhamasisha kujenga uwezo (k.v kiufundi, kifedha na kiuongozi) wa watendaji wanaohusika na maswala ya nyumba na Maendeleo ya Makazi.
Kuhakikisha kuwa mipango, sheria, kanuni za ujenzi, viwango na udhibiti vinalingana na uwezo, mahitaji, matakwa na matarajio ya sekta mbalimbali za wananchi
Kuhamasisha uzalishaji na matumizi ya vifaa vya ujenzi vya hapa nchini na vya gharama nafuu
Kuonyesha kwa vitendo matumizi ya vifaa vya ujenzi vya nchini
Kushauri serikali na wananchi mambo yanayohusu maswala ya maendeleo ya makazi

KWA MENGI ZAIDI KUHUSU WAKALA HUYU TEMBELEA TOVUTI YA NHBRA HAPA

Unataka Kujenga Ukuta Imara wa Nyumba Yako Utakaodumu Muda Mrefu? Soma Hapa.

Mfano wa jengo la ghorofa moja katika hatua za ubunifu. Ukiwa na mahitaji ya kufanya ubunifu wa jengo lako, wasiliana nasi tutakusaidia. 
Mara nyingi tunajenga nyumba zetu za kuishi au kwa shughuli za kiofisi/biashara kwa kutumia malighafi ya tofali. Vipande vya mawe, tofali nk huungwa moja moja juu ya jingine kwa mpishano maalumu kwa kutumia mota ya simenti na mchanga na hatimaye kupata kitu kinachoitwa ukuta wa nyumba. Aghalabu malighafi na aina ya tofali ikawa tofauti kutegemeana na sababu mbalimbali.

Ukuta wa nyumba ni sehemu muhimu na ya kudumu katika jengo lolote. Huweka uimara wa jingo na kudhibiti joto la nje na la ndani sambamba na kuweka usiri wa vitu vilivyomo ndani ya jingo. Hutoa ulinzi au tuseme kuweka usalma dhidi ya matukio ya hatari na wizi kwa vitu ama watu waliomo ndani.

Ukuta tunaouzungumzia hapa ni ule unaoitwa kitaalamu kama ‘masonry wall’ au ukuta wa tope ambao ni matokeo ya utaalamu wa ufundi uashi. Fundi huyu hutumia mota iliyotokana na mchanganyiko wa simenti (au chokaa, udongo nk), mchanga na maji kwa uwiano maalumu kutengeneza kiunganishi (bonding materials). Mchanganyiko huu ukiwa na utepetepe kiasi huunganisha kipande kimoja kimoja cha ama tofali, jiwe, marble, granite, vigae n.k. Tofali linaweza kuwa ama la kuchoma (brick) au yatokanayo na simenti na mchanga pekee au pamoja na kokoto (blocks). 

Yapo majengo yaliyojengwa kwa kuta za zege, mbao au malighafi nyingine. Hatutaweza kutazamia hayo. Tutajikita zaidi kuangazia masonry walls kama nilivyotambulisha awali.

Kwa sehemu kubwa ya ujenzi wetu, katika kujenga ukuta wa tope tunatumia simenti kama kemilikali unganishi muhimu zaidi. Simenti nayo ina ubora tofauti kutegemeana na matumizi. Zipo simenti za aina nyingi kwa matumizi tofauti, tutakuja kuzifahamu wakati mwingine.
Jambo la msingi sana kufahamu, ukuta wa nyumba yako utakuwa imara na wa kudumu zaidi kutegemeana na mambo makubwa matatu
1.   Aina ya ukuta unaojenga, mtindo na muundo wake (ukuta wa mawe, tofali,
2.   Ubora wa malighafi uliyotumia kulingana na hali nyingine za mazingira
3.   Ufundi sahihi katika kujenga ukuta
Kulingana na aina ya malighafi inayotumika kujenga ukuta wa tope, inaweza kuwa ni mawe, tofali n.k tunaweza kupata ubora na uimara tofauti ambao utawezesha kuwako kwa aina mbili kuu za ukuta kutokana na nafasi yake kwenye jengo.
1.   Ukuta unaobeba uzito wa jengo (Load Bearing Masonry Walls)
2.   Ukuta usiobeba uzito wa jengo (Non Load Bearing Masonry Walls)
Aina ya kwanza ya Ukuta unaobeba uzito wa jengo, hujengwa kwa kutumia matofali ya kuchoma, mawe, au matofali ya zege/mchanga. Kazi ya ukuta wa aina hii mbali na kugawanya vyumba na kutoa usiri, hufanya kazi kubwa ya kuchukua na kusafirisha uzito wa paa ama jengo jingine la juu kama ni nyumba ya ghoroa na kuupeleka kwenye msingi wa jengo na hatimaye ardhini.
Mfundi ujenzi wakiendelea na kazi ya ujenzi wa msingi wa nyumba, msingi wa tofali
Kuna unafuu wa gharama kama ukijenga ghorofa kwa kutumia ukuta wa aina hii badala ya nguzo na bimu za zege, hasa kwa jingo la ghorofa moja. Jambo muhimu ni ubora wa malighafi na unene wa ukuta, bila kusahau uwiano wa urefu na unene (slanderness ratio), na huku uimara wa msingi wa jengo katika dhibiti kucheza kwa ardhi kukiwa na umuhimu mkubwa. Kwa hiyo kuta hizi hufanya kazi ya kusafirisha uzito kama mbadala nguzo za zege na nondo. Unafuu unaweza usionekane pia kama eneo unalojenga litalazimu kuwa na msingi wa jamvi nene la zege (raft foundation)
Msingi wa nyumba ukiwa tayari kwa kujenga kuta za kugawanya vyumba. Msingi wa namna hii unauwezo wa kuhimili nguvu zinazoweza kusababisha nyufa. 
Hata hivyo, kuna hatari ya kutokea nyufa kwenye kuta za namna hii kutokana na kukosekana kwa fremu ya nondo na zege ambayo husaidia kukabiliana na nguvu mgandamizo (compression force) na nguvu za utengano (tension forces). Nyufa hizi huwa hatari zaidi kama zitashuka mpaka kuvuka msingi wa jengo.

Mashaka ya jengo kutohimili kutokea kwa nyufa ni hasa wakati wa kukabiliana na matukio kama tetemeko la ardhi, mvua kubwa na upepo mkali, na bila kusahau misukumo ardhini na kuyumba kwa utulivu wa msingi wa jengo (earth pressure & differential foundation settlement). Kufikiria hatari hizi, unalazimika kujihami kwa kushirikisha wataalamu ili kuondokana na mashaka  
Uzito (loads) tunaouzungumzia hapa ni mjumuisho wa uzito wa kuta zenyewe, watu na vilivyomo ndani ya jengo, paa la jengo na nguvu ya upepo (imposed & dead loads). Vipimo vya matofali kwa viwango vyetu ni mm 450x230x150 na mm 450x230x100 ambayo kwa lugha za mafundi huzungumzia inchi 9 (tofali la kulaza), 6, 5 na 4 (tofali la kusimama). Kama utatumia tofali kwa ajili ya ukuta unaobeba uzito, ni wazi kuwa utahitajika kujenga ukuta mnene (tofali za zege za kulaza) ambao utakuwa haupungui mm 225 (inchi 9). Kuta nyingine nyembamba unaweza kuzitumia kwa ajili ya kugawanya vyumba.
Hata hivyo, unene wa ukuta utaongezeka kutegemeana na matumizi ya jengo (occupancy) sambamba na idadi ya ghorofa juu ya “floor” ya chini inayogusana na ardhi.
Kwa ujenzi wa ghorofa, ni sahihi zaidi kujenga kuta za chini kwa mtindo wa mchanganyiko wa tofali pamoja na nguzo chache za zege na nondo zilizoungwa na bimu kuzunguka jengo zima, zikiunganishwa na slabu. Wahandisi wabunifu majengo (Structural/Civil Engineers) wanaweza kukusaidia kupata vipimo sahihi.
Ujenzi wa linta ambayo pia inatumika kuunganisha nyumba nzima kama ring beam. Ni aina ya ujenzi wa kawaida mitaani kwetu na matokeo huwa bora kama mafundi wataalamu watatumika. 
Aina ya pili, Ukuta usiobeba uzito wa jengo ni kuta ambazo kazi yake kubwa ni kugawa vyumba (partition walls) kwa ajili ya usiri na kulinda waliomo ndani dhidi ya hatari za nje. Katika jengo lenye kuta za namna hii kunakuwa na kuta nyingine ama nguzo ambazo ni maalumu kwa ajili ya kusafirisha uzito, mathalani maghorofa mengi tunayoyaona yakijengwa mijini. Kuta hizi hazilazimiki kuwa nene sana na ndio maana unaweza kujenga ukuta wa inchi 4 tu kwa ajili ya kugawanya maeneo ya choo na bafu. 
Mfano wa nyumba ya kuishi iliyokamilika . PICHA ZOTE NI HATI MILIKI YA BLOGU HII

TUNAKOSA NINI TUSIPOTUMIA WATAALAMU KATIKA UJENZI WETU? - PART V: FAHAMU HASARA ZINAZOKUKABILI

KARIBU KATIKA SEMEHU YA MWISHO YA MAKALA YETU INAYOHOJI “TUNAKOSA NINI TUSIPOTUMIA WATAALAMU KWENYE UJENZI WETU?”. 

Sehemu iliyopita tuliweza kuwafahamu baadhi ya wataalamu muhimu katika ujenzi wa nyumba za makazi na biashara, halikadhalika miradi mingine kama ujenzi wa barabara, madaraja na mabwawa ya maji.


Katika kuhitimisha makala yetu hii, leo tutahitimisha kwa kauangalia baadhi ya faida tunazozikosa kwa kutowashirikisha wataalamu katika kufanya miradi yetu ya ujenzi, hasa kwa nyumba zetu za makazi.

Kama zilivyo nchi nyingine zinazoendelea, nchi yetu pia imekuwa ikikabiliwa na upungufu mkubwa nyumba na makazi bora ya watu kuishi. Watu wengi wamejikuta wakijenga kiholela kutokana na sababu mbali mbali zikiwemo za kiuchumi na mamlaka za miji kutowajibika ipasavyo kusaidia jamii kuwa na makazi bora na yanayokidhi mahitaji ya sasa na baadae.


Kushirikisha wataalamu kunatoa fursa ya kujua mbinu mpya na bora za ujenzi, kufaahamu vifaa vya ujenzi na sifa zake, kujua namna ya kupata gharama nafuu za ujenzi na usanifu majengo kuendana na ndoto yako binafsi. Wataalamu wanaposhirikishwa Serikali yetu inakuwa na uhakika kuwa mipango, sheria, kanuni za ujenzi, na viwango vya ujenzi vinazingatiwa ili kuiwesesha kupanga mipango ya kuhudumia jamii yote kwa mahitaji kama miundombinu ya umeme, kukabili majanga ya moto, maji safi na maji taka.

Kama tulivyofahamu awali, Ujenzi ni teknolojia ya kujenga nyumba, viwanda, barabara, daraja au hata miji. Ni kazi inayohusisha wataalamu wengi na ngazi mbalimbali ya kupanga na kutekeleza. Majengo madogo yanajengwa na watu binfasi kufuatana na maarifa yao bila kuhitaji mpangilio mkubwa kwa kutumia mafundi wenye ujuzi kiasi kutoka vyuo vya ufundi au waliojifunza kupitia maarifa ya watu waliowatangulia. Mamlaka ya Mji husika hulazimika kushirikishwa ili kuruhusu mpangilio unaoruhusiwa kisheria.
Miradi mikubwa ya ujenzi huhitaji mpangilio maalumu na ni lazima kwa mwenye jengo kutafuta kwanza ushauri wa wataalamu, ambao watasimamia kazi yake kuanzia mwanzo wa ubunifu mpaka kukamilika kwa ujenzi.

Mhadisi na msanifu majengo watachora michoro ya jengo. Wataalamu wakadiriaji gharama watakadiria mahitaji ya vifaa na gharama za jengo, usimamizi na malipo mengine ya vibali. Watatafutwa wakandarasi ambao watakaa na kupanga mahitaji ya muda, pesa, wafanyakazi na mashine zitakazotumika.
Kisha ujenzi utasimamiwa na mhandisi na msanifu wa jengo pamoja na wataalamu wengine ambao wamesajiliwa na kupewa vibali vya kufanya kazi hiyo na mamlaka husika. Mamlaka ya mji husika nayo itahusika na watu wake wa ardhi na mipango miji. 

Yote yakizingatiwa na kutekelezwa kwa usahihi na uaminifu hitimisho ni kupata jengo zuri na lenye thamani kulingana na gharama zilizotumika, ambayo ni faida kwa mmiliki wa jengo. 

Kwahiyo, ukiachana na utambulisho huo mpana kuhusu majengo makubwa tufikirie sasa kwa udogo wa majenzi yetu ya makazi ya kuishi kwa kuzingatia sharia na taratibu za miji mbalimbali. Ingawa kwa sehemu kubwa nchi yetu ina shida ya maeneo kutopimwa na kutambulika matumizi halali ya ardhi, lakini bado kuna changamoto ya watu wengi kupuuza taratibu zilizopo kwa sababu za kawaida sana.

Kujenga nyumba kunahitaji umakini mkubwa sana na wakati mwingine mwenye kujenga anahitajika kuwepo eneo la ujenzi mara kwa mara na ikibidi kushiriki katika hatua zote za kuanza wazo la ujenzi mpaka kukamilika kwa nyumba yake. Ukaribu huu unakusaidia kupata nyumba na makazi ya ndoto yako.

Kwa kuangalia msingi kwamba atakayeitumia ni wewe na familia yako, ni wazi kuwa unahitaji kuhakikisha unapata makazi yaliyo bora na yatakayodumu kwa muda mrefu. Pengine, yawezekana ukawa huna kabisa ufahamu wowote kuhusu namna ya kufanya ujenzi wako na kuwa vile unavyotamani. Pengo hilo linazibwa na wataalamu wa ujenzi kama ukiamua kuwashirikisha. Hawa watakusaidia kufanya ndoto yako kuwa kweli na kukuongoza kupata bidhaa za gharama nafuu na bora. 


Mtaani kuna mafundi wengi wazuri na wazoefu lakini wana dosari ya kujenga kwa mazoea pekee na kukariri kazi nyingine zilizopita na ndio maana ni rahisi kukuta mitindo ya nyumba iliyojengwa na fundi mmoja ikifanana kwa mambo mengi. Hali itakuwa tofauti kama mafundi hawa watashirikisha ujuzi wao na utaalamu mwingine ili kuweza kufanikisha kile anachohitaji mwenye kutaka nyumba.

Katika kunogesha mada yetu hii, nadhani ni vyema pia tukafahamishana na kujikumbusha baadhi ya mambo muhimu ya kuzingatia wakati wa kujenga nyumba yako kwa upya kabisa, na hasa ikiwa ndio mara yako ya kwanza kufanya ujenzi:


1.    Kuwa na dondoo kadhaa kuhusu gharama za ujenzi
Kabla ya kuanza ujenzi, fanya tathmini binafsi ili uweze kujua kama unaweza kumudu gaharama ya nyumba unayotaka kwa ukubwa gani kwa muda kiasi gani. Mambo mengine ni malighafi utakazotumia na zitapatikana wapi nan i wapi utajenga. Mambo yote haya ukiyatathmini kwa usahihi y1akupa muelekeo wa gharama na jinsi utakavyofanikisha ujenzi wako.

2.    Fahamu aina ya mafundi na wataalamu utakaowahitaji kukujengea
Ni muhimu pia kuwajua mafundi wazuri na unafuu wao wa gharama sambamba na wataalamu washauri na wachora ramani watakaokusaidia hasa kwa miradi mikubwa. Endapo utataka kuuza kazi zote kwa mtu mmoja ni muhimu pia kuwafahmu uwezo wake, gharama, ubora wa kazi afanyazo na uaminifu wake kwenye kazi na usimamizi wa fedha.

3.    Fahamu kuhusu taratibu za kisheria zinazosimamia maswala ya ujenzi katika eneo la Mji unaoishi
Kila mamlaka ya Mji inataratibu zake za upangaji mandhari ya mji wake kwa makazi na matumizi ya umma, viwanda n.k. Ni muhimu kufahamu mamalaka ya eneo husika imepanga matumizi gani kwenye eneo unalotaka kujenga. Idara ya ardhi itathibitisha umiliki wa eneo na uhalali wa matumizi tarajiwa na idara ya ujenzi watakagua michoro kama inakindhi viwango vya ubora na miundombinu ya maji taka na kutoa Kibali cha Ujenzi. Kwa tatizo la kuwa na maeneo mengi yasiyopimwa, Mabaraza ya Ardhi ya Kata husaidia kutoa uthibitisho wa matumizi ya eneo husika kama halijapimwa. Fuata masharti ya ujenzi kuepuka usumbufu usio na sababu.

4.    Fikiria mahitaji halisi na muundo wa nyumba unayoitaka
Kama ni nyumba ya familia au biashara, ni wewe ndiye unayejua mahitaji halisi kwa maana ya idadi ya vyumba, matumizi yake na pengine muonekano unaoutamani. Mbunifu majengo anaweza kukuongoza kupata mchoro mzuri kwa viwango vya nafasi kitaalamu ili kusitokee nyumba ikajenga halafu ikaonekana chumba Fulani ni kikubwa sana au kimepungua. Kwa hiyo katika hatua hii unafanya kama vile ndio uko ndani ya nyumba na unaigiza akilini kama ndio unaona maisha halisi ndani ya nyumba, unaona swichi za umeme na taa zilipo na kukuhudumia vizuri.

5.    Fikiria mandhari ya nje ya nyumba
Watu wengi hasa wanaokopi ramani tu na kujenga wanakosa umaridadi wa mandhari ya nje. Ni vyema sana ukajenga kufuatana na muundo wa kiwanja chako. Kwa hiyo, utaona umuhimu wa kupata mtaalamu akakutengenezea ramani itakayoendana na eneo lako. Kuna mambo ya kuzingatia kama sehemu ya kuegesha gari, kuanikia nguo na shughuli za uwani, mahali pa kupumzikia na watoto kucheza, na namna ya kuingia nyumbani kwako bila kusahau sehemu sahihi ya kuweka mifumo ya maji taka kwa urahisi wa gari la maji taka kufika hasa kama hakuna mfumo wa majai taka wa umma kuweza kuunganisha.
Mandhari ya nje inahusisha ukijani wa miti na maua. Ni muhimu pia kuwazia mambo kama hayo pia.

6.    Fikiria maisha marefu ya jengo lako
Yawezekana unapanga kujenga nyumba yako eneo fulani ukitaraji litakuwa makazi yako ya kudumu. Lakini, uhalisia ni kuwa maisha nayo hubadilika kadiri majukumu ya kiuchumi yanavyobadilika. Ni nyema ukafikiria kuwa na jengo lisilohitaji ukarabati mkubwa kisi cha kuongeza gharama za maboresho huko baadae endapo itatokeo ukalazimika kufanya biashara. Aina ya malighafi utakayotumia pia ina nafasi kubwa kwenye gharama za ukarabati muda baada ya muda.

7.    Fanya uchaguzi mzuri wa finishing materials na decorations

Ni kawaida kukuta nyumba imebuniwa vizuri lakini finishing touch yake na rangi vinafanya iwe ya muonekano usiopendeza. Tumia muda mwingi kupeleleza huku ukishauriana na wataalamu na kusoma majarida mbalimbali ili uweze kupata chaguo sahihi la rangi na malighafi nyingine za kumba nyumba yako kwa ndani na nje. Kuna rangi maalumu kwa ndani pekee na nyingine kwa nje pekee. Halikadhalika madhari ya majirani zako na ukijani uliokuzunguka navyo vinaathiri aina ya urembo wa nyumba. Muhimu kushirikisha wataalamu wa kazi husika kukusaidia mawazo na ushauri.




Kwa hiyo, usiposhirikisha wataalamu katika ujenzi wako unakosa faida zifuatazo:

1.       Kupata aina ya nyumba inayojitosheleza kuendana na matamanio yako. Katika ubunifu kuna mambo usiyoyajua ambayo wataalamu watakusaidia kuyafahamu, matahali uhusiano wa uelekeo wa upepo na milango/madirisha (cross ventilation) n.k. Ukimshirikisha mbunifu akayaweka mawazo yako katika mchoro, atakusaidia kupata picha halisi ya jinsi nyumba yako itakavyokuwa nah ii itakuongezea hamasa ya kukamilisha ndoto yako.



2.       Kujenga kwa ramani/michoro ya nyumba. Michoro hii itakusaidia kwa masuala mengine kama bima, kupata mkopo, kuuza n.k. Itakusaidia pia kama utahitaji kufanya maboresho ya nyumba yako na kuwa rahisi kwa fundi mwingine kujua eneo Fulani kuna nini katika nyumba.

3. Kushirikisha wataalamu kutakusaidia kujua makadirio ya gharama za ujenzi wako. Makadirio haya hayatawezekana kukupa uhalisia kama hutakuwa na michoro yenye vipimo na mapendekezo ya finishing, milango, madirisha, na aina ya uezekaji wa paa. Michoro hii utaipata kwa mbunifu wa majengo endapo utamshirikisha. Ukishakuwa na michoro ya jengo lako, unaweza kuwa kwenye nafasi nzuri zaidi ya kujua ujenge namna gani kwa awamu hasa kama huna nguvu ya kujenga nyumba nzima kwa wakati mmoja. Bila michoro utajikuta unajenga na kuongeza vyumba kwa mpangilio usioshabihiana.

4.       Kushirikisha wataalamu kutakuepusha kujikuta unaingia kwenye hasara ama ya kubomolewa nyumba au kulipishwa faini zisizo za lazima kwa ama kupuuza au kutojua na kufuata utaratibu fulani.  Wakati mwingine ukipata mtaalamu mwaminifu atakusaidia kutotapeliwa na maofisa wasio waaminifu.

5.       Nafasi ya kushauriana na mtaalamu mchoraji namna ya kuongeza au kupunguza ukubwa wa jengo lako wakati ujenzi ukiendelea kwa msingi kwamba wakati wowote mawazo yanaweza kubadilika na kutamani eneo Fulani likae tofauti na lilivyobuniwa awali.

6.       Kama unataka kujenga kwenye eneo ambalo halijapimwa, mtaalamu atakusaidia kupata michoro ya jengo ambayo hata wakati wa ukaguzi wa baadae bado jengo lako litapimwa na kuonekana liko kwenye viwango na kuwa na thamani nzuri.

7.       Kushirikisha wataalamu waaminifu kutakusaidia kuepukana na wachakachuaji wakitumia kigezo cha wewe kutokuwa na ufahamu na mambo ya ujenzi. Kuna baadhi ya wajenzi si waaminifu na wanaweza kukupa hesabu kubwa za vifaa kinyume na uhalisia kwa lengo la kupata faida zaidi.
8.       Kupata kilicho bora na kwa thamani halisi ya fedha zako.

9.       Wataalamu watakusaidia kupata mbadala wa malighafi ya kutumia katika ujenzi wako huku ubora na uzuri wa kazi ukiwa vile vile kama unavyotamani. Hii ni pamoja na ushauri kuhusu malighafi zinazoweza kukuongezea gharama za ukarabati wa nyumba yako mara kwa mara.

10      Wataalamu watakusaidia kujua ukubwa wa chumba kwa matumizi tofauti kuendana na ukuaji wa teknolojia. Mathalani size ya madirisha, milango, vitasa na hata ukubwa wa maeneo kama choo na bafu ili kutosheleza vifaa utakavyonunua kwa ajili ya matumizi yako. Hata namna ya kupanga sebule kisasa kwa uwiano mzuri na sebule, jiko na veranda ni mambo ambayo utayapata kwa ushauriano mzuri na mtaalamu wa ujenzi.

11      Kuepuka hasara ya kujenga nyumba kubwa isiyosadifu mahitaji halisi kwa mhusika kutofahamu namna ya kujenga kulingana na mahitaji ya wakati gani.

Nyumba iliyojengwa kwa kubuniwa vizuri huleta raha kuishi ndani yake maana inakuwa na mpangilio unaotoa uhuru kwa kila memba wa familia kufurahia eneo lake na kuweka usiri wa mambo ya familia na wageni. Unaweza kujiuliza, kuna sababu yeyote ya msingi kwa mtu anayejenga nyumba ya milioni 65 lakini anakwepa kupata michoro kwa gharama ya shilingi laki tano tu au hata pungufu?

Kumbuka, katika ujenzi wa nyumba, kosa likishafanyika awali na nyumba kukamilika ni gharama sana kurekebisha. 


Mwandishi/Mchambuzi
Tumainiel W. Seria
BSc. Building Economics (Hons), UCLAS
GQS (Registered with AQRB)
Blogger (http//:arusha255.blogspot.com na http//:ujenzidirect.blogspot.com)
Project QS, Proposed PPF Plaza Corridor Area Arusha
P.O Box 16094 Arusha
+255757718080
seria.tw@gmail.com

TUNAKOSA NINI TUSIPOTUMIA WATAALAMU WAUJENZI? - PART IV: WAJUE WATAALAMU KWENYE SEKTA YA UJENZI

KARIBU TENA KWENYE MAKALA YETU YA 'TUNAKOSA NINI TUSIPOWATUMIA WATAALAMU KWENYE UJENZI WETU?' SEHEMU YA NNE

Tuwajue wataalamu wetu wa ujenzi.

Ndugu msomaji wangu, nikushirikishe sasa kuweza kuwafahamu wataalamu mbalimbali walio na taaluma anuai kuhusiana na masuala ya ujenzi wa majumba. Ni jambo jema kufahamu kuwa wataalamu wote hawa wamesomeshwa na vyuo vyetu vya hapa nchini. Hii ni kusema kwamba utaalamu wa ujenzi ni wetu wenyewe ingawa kwa upande wa bidhaa za ujenzi bado tunategemea sehemu ya utaalamu na ubunifu wa nje ya nchi.

Sote tu mashahidi wa namna taifa la China na raia wake walivyosambaa barani Afrika na Tanzania ikiwemo kutafuta masoko ya bidhaa zao za ujenzi.

NSSF Mafao Haouse, Arusha (Designed by MD Consultancy Ltd)

Wataalamu wengi wa ujenzi nchini wanapata mafunzo yao kwenye taasisi za elumu ya juu kama ATC (Arusha Technical College), MIST (Mbeya Institute of Science and Technology), DIT (Dar es Salaam Institute of Science and Technology), ARU (Ardhi University), CoET n.k; vituo vya mafunzo vya VETA na baadhi ya shule za ufundi kama “Moshi Tech” n.k. 


Shughuli nzima ya ujenzi nchini inasimamiwa na Serikali kupitia Wizara husika na mamlaka zake; na pia Bodi mbalimbali kama Bodi ya maiinjinia-ERB, Bodi ya wakandarasi-CRB, Bodi ya Wakadiriaji Majenzi na Wabunifu Majengo-AQRB bila kuwasahau Baraza la Ujenzi la Taifa-NCC na kwa miundombinu wanaongezeka wakala wa barabara nchini – TANROADS na TARURA.

Ni kina nani na yapi majukumu ya wataalamu (proffesionals) kwenye “kiwanda” cha ujenzi nchini?

Hili ni swali zuri na muhimu ambalo litatuongoza kuwafahamu na kuyafahamu majukumu yao katika ustawi wa sekta ya ujenzi nchini. Baadhi hatuwaoni kwenye ujenzi wa majumba yetu ya kuishi lakini wanafanya kazi katika maeneo mengine makubwa zaidi. 


Tuanze na timu ya wataalamu wanaotambulika kitaaluma kama Geotechnic Engineers (GE). Mpangilio wa masimulizi hautafuata ubora ama umuhimu wa kila taaluma. GE, hawa ni wataalamu wanaohusika na kuchambua sifa za udongo kama sehemu ya taaluma ya uinjia wa majenzi ya barabara, madaraja, mifereji, mabwawa na majengo makubwa, ambapo taaluma hiyo inajulikana kama Civil Engineering.

Mhandisi udongo/Geotechnic Engineer 

Huyu anafanya kupembua sifa za udongo za kimuonekano, kikemikali ambazo zinaweza kuathiri mradi wa ujenzi na namna jingo linavyoweza kukabiliana na matetemeko ya ardhi na majanga mengine na hatimaye kupata muafaka wa aina ya msingi (foundation) wa jengo, daraja n.k unavyopaswa kuwa.

Land Surveyor/mpima ardhi. 
Hili ni kundi linguine la wataalamu wa maswala ya kupima ardhi na mara nyingi wanakuwa sehemu ya utendaji wa kiSerikali. Wizara ya Ardhi, Nyumba na Makazi na Halmashauri za Miji na Majiji ndipo mahali hasa unaweza kuwakuta wataalamu hawa kama maafisa ardhi. Hata hivyo zipo kampuni binafsi pia zinazotoa huduma za upimaji ardhi na wataalamu hawa wanapatikana huko pia.

Kazi yao kubwa katika sekta ya ujenzi kama wataalamu wa kwanza kabisa kufanya kazi eneo la ujenzi kabla ya wengine ni kutambua mipaka ya eneo la ujenzi, kutambua ukubwa wa eneo, kuweka na kukagua beacons, bila kusahau kutambua kiasi cha mbonyeo au mwinuko wa ardhi inayotarajiwa kujengwa. Kazi za taalumu hii zimekuwa zikitolewa zaidi kwa muda mrefu katika Chuo Kikuu cha Ardhi, Dar es Salaam.

Mbunifu majengo/Architect

Huyu ndie mtaalamu aliyefuzu mafunzo na kusajiliwa kubuni michoro ya jengo kwa kubadilisha mawazo (concepts) ya mradi fulani na kuyaweka kwenye michoro na muonekano wa uhalisia wa jingo litakavyokuwa likishajengwa. Hufanya kutafsiri mahitaji ya anayetaka kujenga na kuyaweka kwenye uhalisia kwa namna ya kumuwezesha mjenzi kufanya ujenzi.  Hutengeneza taswira ya muonekano wa jengo na mpangilio wa mambo mengine. 

Kabla ya kuanza ujenzi, mbunifu huyu anatakiwa kuchora mchoro wa jingo husika na ndipo ujenzi uanze. Ni rahisi kukosa mwelekeo wa ujenzi kama utaanza kazi ua ujenzi ukiwa huna mchoro unaokuongoza. 

Taaluma ya ubunifu majengo ama Architecture kama taaluma nyingine nayo ina mgawanyo wa utaalamu kwa maana ya ubunifu wa ndani ‘interior design’, mpangilio wan je ya jingo na vitu nama bustani na sehemu za maegesho ‘landscaping’ na ubunifu wenyewe wa jango zima na umaridadi wake wan je na mgawanyo wa vyumba na maeneo huru ndani. 

Bado ni vyuo vikuu vichache ambavyo vinatoa mafunzo ya taaluma hii hapa nchini ambapi pia kuna mafunzo ya wasaidizi kwa ngazi za chini ambao nao hufanya kazi za uchoraji pamoja, kitaalamu hutambulika kama draughtsmen.


Wahandisi/(Civil and Structural Engineers)
Baada ya Mbunifu majengo kumaliza kazi ya kuandaa michoro yake mhadisi ndiye mtaalamu wa pili kuweka utaalamu wake. Mara nyingi kumekuwapo na mchanganyo wa uhandisi na ukandarasi. Kuweka hili sawa kupitia makala hii, ifahamike kuwa mhandisi ni mtaalamu mbunifu wa uimara wa jingo na mkandarasi ni mjenzi wa jingo akifanyika kazi vilivyobuniwa na wahandisi na wabunifu majengo. Mkandarasi anaweza kuwa aidha mtu binafsi au kampuni iliyosajiliwa kufanya kazi ya ujenzi kwa kiwango fulani.

Sasa huyu anayejulikana kama Structural Engineer ndiye Mhandisi hasa na huwajibika kwa uhandisi wa ubora na uimara wa jengo kwa kufanya mahesabu ya uimara (strength), uzito, nguvu na namna vitakavyokabiliana bila kuleta madhara kwenye jengo linalotarajiwa kujengwa.

Ni jukumu la mhandisi huyu kuandaa michoro ya uimara wa jengo kwa maana ya namna nondo na zege na hata vyuma vingine vitakavyokuwa na ukubwa wake kwa maeneo kama nguzo (column), msingi (foundation) bimu (beams), kuta, ngazi za ghorofa na slabu (slabs) kwa upande wa majumba. Halikadhalika huandaa michoro kwa ajili ya madaraja, nguzo kubwa, mabwawa n.k. 

Wakati wa ujenzi anakagua pia ubora wa bidhaa (materials) zinazotumika na namna nondo na zege zinavyotengenezwa kama vinafikia ubora unaotakiwa kama alivyobuni kimahesabu.

Inapotokea jengo limeanguka kwasababu zisizotokana na nguvu za asili kama mtetemeko ya ardhi na milipuko ya bomu kwa mfano, mhandisi ndiye hupewa majukumu ya kuchunguza sababu za kihandisi zilizopelekea hitilafu iliyosabababisha jengo kuanguka kama iivyotokea maeneo ya Kisutu Jijini Dar es Salaam miaka michache iliyopita. 

Mkadiriaji Majenzi/Quantity Surveyor(QS)
Mkadiriaji majenzi kwa baadhi ya nchi hutambulika kama Cost Engineer. Ni sawa na kusema ndiye mhasibu kwenye sekta ya ujenzi. 

Majukumu makubwa ya mkadiriaji majenzi ni kufanya makadirio ya gharama za mradi wa ujenzi. Makadirio hufanyika wakati wa kubuni wazo la mradi, wakati wa ujenzi na wakati wa kuandaa mkataba wa ujenzi kwa ajili ya kupatana na mkandarasi. Makadirio haya hufanyika kimahesabu kwa majengo mapya au yanayokarabatiwa ama kuboreshwa. 

Mkadiriaji majenzi hufanya kazi katika sekta zote mpaka kwenye uchimbaji madini, miundombinu, na majengo ya nyumba za kuishi na majengo makubwa ya viwanda na taasisi za umma au jumuia. Ili kuweza kukamilisha kazi yake hulazimika kutafuta kiasi (quantity) cha visaidizi kama nguvu kazi, zana za kazi, bidhaa za ujenzi n.k. 

Katika miradi mkubwa ya ujenzi QS ndiye huwajibika kufanya yafuatayo
a. Kufanya makadirio ya bajeti ya mradi
b. Kuchanganua madhara yanayoweza kujitokeza kwa kubadilisha dizaini ya jengo na bajeti yako
c. Kuandaa BOQ (kitabu cha makadirio ya gharama na kiwango cha kazi) ambayo husaidia wakati wa kumtafuta mkandarasi wa kutekeleza ujenzi
d. Kuandaa kamabrasha ya tenda za ujenzi na kusimamia zoezi zima
e. Kuhakiki kazi ya ujenzi iliyofanyika na kuipa thamani yake kwa ajili ya kuruhusu malipo kufanyika kwa mkandarasi kwa kiwango cha kazi alichofanya.
f. Kusimamia mabadiliko yate ya kimuundo na kiujenzi na hata gharama wakati ujenzi unaendelea tofauti na kilichobuniwa awali.
g. Kuandaa hesabu za malipo ya mwisho kwa makandarasi ilikwa mmradi umekamilika kwa namna taratibu na sharia za ujenzi zinavyoelekeza na majukumu mengine. 

Mjenzi/Builder
Mjenzi au builder husoma na kuielewa michoro yote na maelekezo mengine na kuangalia inaoana vipi. Anachanganua uwezekano wa jengo kujengeka na namna litakavyotunzika kama lilivyobuniwa. Ni sawa na kusema huyu ni mhakiki ingawa kwa hapa kwetu ni nadra kuwakuta wataalamu hawa kwa majukumu haya kama mtaalamu wa pembeni. Mara nyingi wanakuwa kama sehemu ya wakandarasi.

Mhandisi wa Huduma za Jengo/(Building Service Engineer)
Kwa kawaida jengo halikamiliki kwa kuwa na ubunifu wa jengo lenyewe tu na uimara wake. Kwasababu kila jengo ni maalumu kwa matumizi Fulani huwa kunakuwa na huduma muhimu za kuwawezesha watumiaji wa jengo hilo kuweza kulitumia. Huduma tunazozizungumzia hapa ni kama mfumo wa maji safi na machafu, mfumo wa umeme, mfumo wa mawasiliano ya kitekinohama nausalama.

Huduma nyingine ni mfumo wa kukabiliana na hitilafu ya moto, mfumo wa usafirishaji kwenda na kutoka ghorofani (vertical transportation) na mfumo wa kuweka hali ya ujoto au baridi na kutoa hewa chafu nje ya jengo (mechanical ventilation)

Huduma zote hizi hubuniwa na kusimamiwa na mtaalamu anayetambulika kama Mhandisi wa Huduma za Jengo (Services Engineer) akifanya kazi kwa ushirikiano wa karibu na wataalamu wengine ambao nimeshawaelezea hapo awali. 



Mafundi au Artisans
Hawa ndio watu wanaofanya kazi kwa vitendo eneo la ujenzi wakiwa na ujuzi wa namna tofauti tofauti. Mafundi mchundo (Technicians) wanaingia kundi hili pia wakiwa na utaalamu (skills) kwa maeneo tofauti tofauti ya ujenzi kama ufundi seremala, ufundi chuma, ufundi tope (masonry) n.k. 

Wataalamu Washauri (The Consultants)
Kila mradi uliofuata taratibu za ujenzi kwa mujibu wa sharia zetu unalazimika kuwa na timu ya washauri wataalamu kwa msingi kwamba mmiliki (Client) anayetaka kufanya maradi wa ujenzi anaweza kuwa sio mtaalamu wa maswala ya ujenzi na hata akama atakuwa na utaalamu hataweza kuwa na uelewa wa kila kitu. Hivyo inamlazimu kuwa na timu ya watu watakaomshauri na kumsaidia kufanikisha mradi wake ili aweze kupata thamani halisi ya alichowekeza na kilichojengwa kama vinawiana. 

Wataalamu Washauri ni mjumuiko wa wataalamu wote niliowaeleza hapo mwanzo, wataalamu kama Mbunifu Majengo, Mkadiriaji majenzi, Wahandisi wa jengo na Huduma, na wataalamu wengine. 

Hawa washauri wanatakiwa kushirikishwa kuanzia mwanzo kabisa wazo la mradi linapoanza kwsasababu kimajukumu washauri hawa ndio huchukua nafasi ya mmiliki au tajiri wa mradi na kumuwakilisha katika maswala ya kitaalamu. 

Mkandarasi/Building Contractor
Mkandarasi kwa lugha rahisi anahesabika kuwa ni mkusanyiko wa timu ya wajuzi wa masuala ya ujanzi pamoja ambao wao majukumu makubwa ni kubadilisha michoro na kuifanya kuwa uhalisia wa kilichobuniwa. Mkandarasi huwajibika kukusanya vifaa na bidhaa za ujenzi na kutumia utaalamu wa watu wake kufanikisha ujenzi husika mpaka kukamilika kwake na kuwa tayari kwa matumizi yaliyokusudiwa. Kawaida katika miradi mingi kunakuwa na Mkandarasi mkuu na wakandarasi wadogo ambao kwa magawanyo wa majukumu wao hufanya shughuli nyingine ambazo wengine hawawezi. Ndio haswa wanaohusika na ufanikishaji wa huduma za jengo kama nilivyozifafanua awali.

Mkandarasi ninayemzungumzia hapa kisheria ni yule ambaye amepata leseni ya kufanya kazi kutoka Bodi ya Makandarasi nchini (Contractors Registration Board).

Mpaka kufikia hapa ni matumaini yangu kuwa kwa kiasi Fulani nimeweza kudadavua maswala machache muhimu ambayo kimsingi yanatoa jibu la tunakosa nini tusipotumia wataalamu kwenye ujenzi wa nyumba zetu. Kama umebahatika kupeleleza nyumba zilizojengwa kwa kushirikisha wataalamu hata kwa hatua mojawapo na zile ambazo zimejengwa bila kuwashirikisha utakubaliana name kuwa zilizoshirikisha wataalamu zinaubora na umaridadi mzuri tofauti na zile ambazo hazikuhusisha wataalamu hata kwa ushauri tu. 

Tukutane tena katika sehemu ya mwisho ya mfululizo wa makala hii ambapo tutaweza kufahamu sasa nini tunachokikosa. 


Mwandishi/Mchambuzi
Tumainiel W. Seria
BSc. Building Economics (Hons), UCLAS
GQS (Registered with AQRB)
Director: S&L CostCare and Planners
P.O Box 16094 Arusha
+255757718080
seria.tw@gmail.com

TUNAKOSA NINI TUSIPOTUMIA WATAALAMU KWENYE UJENZI WETU? - PART III: SOMA HAPA UNACHOTAKIWA KUFANYA UKITAKA KUJENGA NYUMBA KISASA



ILIPOISHIA SEHEMU YA TATU


Hebu fikiria kwamba ni wewe msomaji wangu umeamua kujiwekea mipango ya kuwa na nyumba yako nzuri, salama na bora. Katika hatua hii ni muhimu sana kujua mambo muhimu yatakayokuwezesha kutimiza ndoto yako ya kuwa na nyumba bora katika makazi bora pia. Kuna orodha ya maaandalizi muhimu yatakayofanikisha ujenzi wa nyumba bora. 

Kwa upana wa makala hii sitazungumzia kwa undani sana mahitaji ya ndani ya nyumba ikiwa tayari kwa matumizi. Nitaangalia zaidi mambo makubwa ya nje ya kufanyia kazi kujiandaa ili kuwa na nyumba ama makazi yaliyobora.

Mfano wa ramani ya nyumba


Jambo la kuanza nalo ni kufikiria mahali sahihi utakapo jenga nyumba yako


Mahali unapotamani kujenga makazi yako yanahusika kuamua aina ya nyumba yako hapo baadae. Inaweza kuwa unawazia kujenga nje ya mji au mjini. Eneo unalotamani kujenga nyumba ya kuishi linaweza kuwa ni eneo lililopimwa ama bado halijapiwa. Ardhi yake ni ya mabonde na milima ama tambarare. Utaangalia matumizi mengine ya eneo hilo na miundombinu yake. Pengine ni eneo jirani na viwanda n.k. Hata udongo na hali ya hewa ya eneo husika inanafasi yake, pengine ni ufukweni mwa bahari.

Kumbuka, uamuzi wa eneo la kujenga unaweza kuashiria uharaka wa kukamilisha kujenga nyumba yako kwasababu kwa mfano kama unatazamia kujenga katika eneo la katikati ya mji huwa ni gharama kubwa na hata upatikanaji wake ni wa taabu kidogo. Ikiwa ni eneo la mjini kuna ugumu wake pia kwa mfano kupata kibali cha kujenga.Miji mingine kwa mfano Jiji letu la Arusha halitoi vibali kwa ujenzi wa nyumba ndogo zisizo za ghorofa kwa maeneo ya katikati ya Jiji.


Kwa eneo ambalo limekwishajengwa na kupangwa kuwa eneo la makazi huwa ni rahisi zaidi hata kupata kibali cha ujenzi wa makazi na miundombinu yake huwa maalumu kwa makazi ya watu.


Jambo la pili kujiandaa nalo ni pesa za kugharamia ujenzi husika hata kwa kuanzia tu na wataalamu utakaowatumia bila kusahahu gharama za mamlaka ya mji au mtaa husika na tozo za vibali mbalimbali vya huduma na ruhusa. Ni vizuri kupanga kiasi cha fedha ulichonacho au kujikusanyia kitakufikisha wapi katika ujenzi wako. Itakuwa gharama zaidi kama utaamua kupata eneo na kujenga hapo hao, ingawa kwa baadhi wanaweza.

Hata hivyo, kutokuwa na pesa ya kuanza ujenzi hadi kumaliza hakuwezi kuwa kizuizi cha kutojenga nyumba iliyobora. Kamwe usikate tamaa ama kuamua kujenga tu alimradi umejenga kitu ambacho hakina ubora na hakikidhi mahitaji kitaalamu. Kuna taasisi nyingi za mikopo (loans and mortgages) zinaweza kukusaidia. 

Lakini pia kwa kujikusanyia pesa kidogokidogo na kuzitunza kwa malengo ya ujenzi unaweza kufanya ujenzi wako ulio katika ubora mzuri. Kuna wataalamu washauri wa maswala ya gharama za ujenzi kabla, baada na wakati wa ujenzi wanaweza kusaidia. Kitaalamu wanaitwa  Quantity Surveyors ama Cost Engineers kwa baadhi ya nchi kama Uingereza.

Hatua ya ya tatu, baada ya kuwa umejiandaa kifedha na maandalizi mengine kufanya ujenzi, fikiria sasa kumpata mtaalamu mbunifu wa majengo atakayekusaidia kuandaa mchoro wa nyumba yako. Hatua hii ni muhimu zaidi na ndipo watu wengi wanapokosea na kujikuta wakitumia gharama kubwa baadae kujenga nyumba ambayo haiwapi raha waliyoitamani kwa kuwazia ama kwa kuona mahali fulani ama kwenye mitandao ya internet. Shirikiana na mchoraji akuelekeze namna ambavyo mawazo yako ameyaweka kwenye mchoro kama unavyohitaji na kuhakiki ukubwa wa nyumba na mgawanyo wa vyumba.

roof structure - seriajr
Jengo kwa matumizi ya kuishi likiwa katika hatua za uezekaji
Kuna baadhi ya watu wanaweza kuona muonekano wa nyumba kwa nje wakavutiwa nao na kumuonesha fundi mjenzi na kumtaka awajengee wakiamini kwa muonekano wa nje watapata kuridhika hata na ndani. Bahati mbaya wanakuwa hawafahamu kuwa mgawanyo wa vyumba ndani, saizi yake na mpangilio wa mahusiano ya vyumba na maeneo tofauti ndio huleta mvuto, ubora na raha ya nyumba husika.

Kwa hiyo, kama nilivyoeleza kuwa ukishakuwa umejiandaa unamtafuta mtaalamu mbunifu wa majengo, kitaalamu anaitwa Architect (tutajifunza baadae nafasi yake katika ujenzi pamoja na wasaidizi wake). Unampatia mahitaji yako halisi na namna unavyotamani nyumba yako iwe, nae kwa utaalamu wake atakushauri namna nzuri ya kuyapanga mahitaji yako hayo na kuyaweka kwenye mchoro ambao fundi anaweza kuutumia kujenga nyumba yako.

Mtaalamu huyo atayaunganisha mahitaji yako na kuyapanga kitaalamu ili kuweza kupata jengo ambalo litakuwa na sifa za mahitaji ya nyumba bora. Mifano ya mahihaji muhimu ni madirisha yanayoruhusu hewa kwa kupangilia uhusiano mzuri na milango kupata kitu kinachoitwa kitaalamu kama cross ventilation. Pia mpangilio wa vyumba, sehemu ya chakula, jiko na vyoo bila kusahau baraza na korido.


Utoaji na uingizaji wa maji masafi na machafu una umuhimu wake pia na halikadhalika namna sebule itakavyokaa na kutumiwa na wageni na watu watakaokuwa wanaishi kwenye hiyo nyumba bila kusahau maliwato kwa mgeni. Pia maswala ya usalama wa jengo dhidi ya hatari ya moto na hata mpangilio wa madirisha kuoanish na uelekeo wa upepo.

Ni vizuri pia tukifahamishana kuwa kwa mujibu wa sheria zetu za ujenzi hapa nchini kuhusu nyumba za kuishi (residential houses), endapo mtu anajenga jengo la ghorofa analazimika kumtafuta injinia amsaidie kumuandalia mchoro utakaohusu uimara wa jeingo kwa maana kwamba utakuwa ni mchoro unaoonesha namna nondo zitakavyojipanga, idadi na saizi yake, bila kusahahu ubora wa zege na mambo mengine yahusuyo uimara wa jingo lako.

Sasa kama utakuwa unawazia jengo la namna hiyo ni lazima kisheria kutafuta Structural Engineer akusaidie kuandaa michoro mingine.


Hatua ya nne, baada ya kuwa na mchoro wako utahitaji kujua makisio ya gharama halisi za mradi ama kwa kujenga mpaka kumaliza ama kwa awamu tofauti. Mtaalamu mkadiriaji majenzi niliyemueleza hapo awali kuwa anatambulika kitaaluma kama Quantity Surveyor/Cost Engineer atahitajika kufanya hesabu za makadirio ya gharama ili uweze kujua namna halisi ya kujipanga kutegemeana na mchoro ulivyo na jinsi utakavyokuwa umechagua material gani za kutumia kwa kushauriana na kitaalamu. QS huyu atakusaidia kubajeti vizuri na kuondoa matumizi yasiyo ya lazima au bidhaa bora na rahisi lakini lengo likibaki kupata nyumba bora. Wakati mwingine hata fundi mzoefu anaweza kukusaidia.

Hatua ya tano. Mpaka hapo utakuwa umeshakamilisha hatua za awali muhimu kabla ya kuanza mradi wako wa ujenzi. Sasa unaweza kuwatafuta wataalamu wajenzi kwa maana ya kampuni au mafundi binafsi wenye uelewa mzuri wa kutafsiri michoro ya ujenzi ili muweze kukubaliana na kuanza kazi ya ujenzi tukichukulia kuwa eneo tayari lipo, limehakikiwa na kuonekana liko tayari kwa ujenzi na udongo wake ukiwa umeshaoanishwa na aina ya msingi wa nyumba utakavyokuwa.

nembo ya AQRB
Sheria Na. 4 ya mwaka 2010 ya AQRB, Bodi ya Wakadiria Majenzi na Wabunifu wa Majengo inahimiza matumizi ya kampuni za wakandarasi zilizosajiliwa kufanya ujenzi kwa kufuata mchanganuo ufuatao

· Ujenzi wa majengo yoyote ya ghorofa ya ukubwa na thamani yeyote
·  Majenzi yote ya makazi yanayozidi thamani ya sh milioni 50 na ujenzi wake unahitaji uhandisi (structural inputs)
· Ujenzi wa majengo yote ya umma kama shule, hospitali, masoko, makanisa, misikiti, kumbi za starehe n.k


·  Ujenzi wa majengo ya viwanda, maghala n.k

Kwa hiyo utaona ni namna gani sheria inajaribu kumsaidia mjenzi kupata kilicho bora kwa kutumia wataalamu. Ni ukweli kwamba idadi kubwa ya watanzania hawana uwezo wa kujenga kwa kutumia wataalamu na hata kiwango cha nyumba yenye thamani ya milioni 50 wakati wa kuanza ujenzi hawana. Baadhi wanazikwepa kampuni wakijaribu kuokoa gharama za ziada ili zitumike kwenye ujenzi wenyewe.
Sehemu ya kazi za kweka urembo wa nyumba kwa ndani. Kazi ya SeriaMjenzi
Hata hivyo, kutokuwa na uwezo wa kukodi ama kuajiri kampuni kufanya ujenzi wako sio kipingamizi cha kutowashirikisha wataalamu kama nilivyoeleza hapo awali. 

Unaweza kuepuka kutumia kampuni kujenga lakini kama uliwashirikisha wataalamu kuandaa wazo la ujenzi wako kitaalamu unaweza kumtumia fundi yeyote mjuzi akakusaidia kujenga kwa gharama ambazo mara nyingi ni pungufu kidogo ya gharama za makampuni. Mtaani tunao mafundi wengi na wataalamu baadhi wakiwa wamehudhuria mafunzo rasmi chuoni na wengine wakijifunzia tu mtaani na kujikusanyia uzoefu. Wote ni wataalamu. 


Itaendelea Sehemu ya nne, ambapo tutaweza kuwajua wataalamu mbalimbali wanaohusikana ujenzi.

Mwandishi/Mchambuzi
Tumainiel W. Seria
BSc. Building Economics (Hons), UCLAS
GQS (Registered with AQRB)
Director: S&L CostCare and Planners
P.O Box 16094 Arusha
+255757718080 seria.tw@gmail.com