Header Ads

Header Ads

TUNAKOSA NINI TUSIPOTUMIA WATAALAMU WAUJENZI? - PART IV: WAJUE WATAALAMU KWENYE SEKTA YA UJENZI

KARIBU TENA KWENYE MAKALA YETU YA 'TUNAKOSA NINI TUSIPOWATUMIA WATAALAMU KWENYE UJENZI WETU?' SEHEMU YA NNE

Tuwajue wataalamu wetu wa ujenzi.

Ndugu msomaji wangu, nikushirikishe sasa kuweza kuwafahamu wataalamu mbalimbali walio na taaluma anuai kuhusiana na masuala ya ujenzi wa majumba. Ni jambo jema kufahamu kuwa wataalamu wote hawa wamesomeshwa na vyuo vyetu vya hapa nchini. Hii ni kusema kwamba utaalamu wa ujenzi ni wetu wenyewe ingawa kwa upande wa bidhaa za ujenzi bado tunategemea sehemu ya utaalamu na ubunifu wa nje ya nchi.

Sote tu mashahidi wa namna taifa la China na raia wake walivyosambaa barani Afrika na Tanzania ikiwemo kutafuta masoko ya bidhaa zao za ujenzi.

NSSF Mafao Haouse, Arusha (Designed by MD Consultancy Ltd)

Wataalamu wengi wa ujenzi nchini wanapata mafunzo yao kwenye taasisi za elumu ya juu kama ATC (Arusha Technical College), MIST (Mbeya Institute of Science and Technology), DIT (Dar es Salaam Institute of Science and Technology), ARU (Ardhi University), CoET n.k; vituo vya mafunzo vya VETA na baadhi ya shule za ufundi kama “Moshi Tech” n.k. 


Shughuli nzima ya ujenzi nchini inasimamiwa na Serikali kupitia Wizara husika na mamlaka zake; na pia Bodi mbalimbali kama Bodi ya maiinjinia-ERB, Bodi ya wakandarasi-CRB, Bodi ya Wakadiriaji Majenzi na Wabunifu Majengo-AQRB bila kuwasahau Baraza la Ujenzi la Taifa-NCC na kwa miundombinu wanaongezeka wakala wa barabara nchini – TANROADS na TARURA.

Ni kina nani na yapi majukumu ya wataalamu (proffesionals) kwenye “kiwanda” cha ujenzi nchini?

Hili ni swali zuri na muhimu ambalo litatuongoza kuwafahamu na kuyafahamu majukumu yao katika ustawi wa sekta ya ujenzi nchini. Baadhi hatuwaoni kwenye ujenzi wa majumba yetu ya kuishi lakini wanafanya kazi katika maeneo mengine makubwa zaidi. 


Tuanze na timu ya wataalamu wanaotambulika kitaaluma kama Geotechnic Engineers (GE). Mpangilio wa masimulizi hautafuata ubora ama umuhimu wa kila taaluma. GE, hawa ni wataalamu wanaohusika na kuchambua sifa za udongo kama sehemu ya taaluma ya uinjia wa majenzi ya barabara, madaraja, mifereji, mabwawa na majengo makubwa, ambapo taaluma hiyo inajulikana kama Civil Engineering.

Mhandisi udongo/Geotechnic Engineer 

Huyu anafanya kupembua sifa za udongo za kimuonekano, kikemikali ambazo zinaweza kuathiri mradi wa ujenzi na namna jingo linavyoweza kukabiliana na matetemeko ya ardhi na majanga mengine na hatimaye kupata muafaka wa aina ya msingi (foundation) wa jengo, daraja n.k unavyopaswa kuwa.

Land Surveyor/mpima ardhi. 
Hili ni kundi linguine la wataalamu wa maswala ya kupima ardhi na mara nyingi wanakuwa sehemu ya utendaji wa kiSerikali. Wizara ya Ardhi, Nyumba na Makazi na Halmashauri za Miji na Majiji ndipo mahali hasa unaweza kuwakuta wataalamu hawa kama maafisa ardhi. Hata hivyo zipo kampuni binafsi pia zinazotoa huduma za upimaji ardhi na wataalamu hawa wanapatikana huko pia.

Kazi yao kubwa katika sekta ya ujenzi kama wataalamu wa kwanza kabisa kufanya kazi eneo la ujenzi kabla ya wengine ni kutambua mipaka ya eneo la ujenzi, kutambua ukubwa wa eneo, kuweka na kukagua beacons, bila kusahau kutambua kiasi cha mbonyeo au mwinuko wa ardhi inayotarajiwa kujengwa. Kazi za taalumu hii zimekuwa zikitolewa zaidi kwa muda mrefu katika Chuo Kikuu cha Ardhi, Dar es Salaam.

Mbunifu majengo/Architect

Huyu ndie mtaalamu aliyefuzu mafunzo na kusajiliwa kubuni michoro ya jengo kwa kubadilisha mawazo (concepts) ya mradi fulani na kuyaweka kwenye michoro na muonekano wa uhalisia wa jingo litakavyokuwa likishajengwa. Hufanya kutafsiri mahitaji ya anayetaka kujenga na kuyaweka kwenye uhalisia kwa namna ya kumuwezesha mjenzi kufanya ujenzi.  Hutengeneza taswira ya muonekano wa jengo na mpangilio wa mambo mengine. 

Kabla ya kuanza ujenzi, mbunifu huyu anatakiwa kuchora mchoro wa jingo husika na ndipo ujenzi uanze. Ni rahisi kukosa mwelekeo wa ujenzi kama utaanza kazi ua ujenzi ukiwa huna mchoro unaokuongoza. 

Taaluma ya ubunifu majengo ama Architecture kama taaluma nyingine nayo ina mgawanyo wa utaalamu kwa maana ya ubunifu wa ndani ‘interior design’, mpangilio wan je ya jingo na vitu nama bustani na sehemu za maegesho ‘landscaping’ na ubunifu wenyewe wa jango zima na umaridadi wake wan je na mgawanyo wa vyumba na maeneo huru ndani. 

Bado ni vyuo vikuu vichache ambavyo vinatoa mafunzo ya taaluma hii hapa nchini ambapi pia kuna mafunzo ya wasaidizi kwa ngazi za chini ambao nao hufanya kazi za uchoraji pamoja, kitaalamu hutambulika kama draughtsmen.


Wahandisi/(Civil and Structural Engineers)
Baada ya Mbunifu majengo kumaliza kazi ya kuandaa michoro yake mhadisi ndiye mtaalamu wa pili kuweka utaalamu wake. Mara nyingi kumekuwapo na mchanganyo wa uhandisi na ukandarasi. Kuweka hili sawa kupitia makala hii, ifahamike kuwa mhandisi ni mtaalamu mbunifu wa uimara wa jingo na mkandarasi ni mjenzi wa jingo akifanyika kazi vilivyobuniwa na wahandisi na wabunifu majengo. Mkandarasi anaweza kuwa aidha mtu binafsi au kampuni iliyosajiliwa kufanya kazi ya ujenzi kwa kiwango fulani.

Sasa huyu anayejulikana kama Structural Engineer ndiye Mhandisi hasa na huwajibika kwa uhandisi wa ubora na uimara wa jengo kwa kufanya mahesabu ya uimara (strength), uzito, nguvu na namna vitakavyokabiliana bila kuleta madhara kwenye jengo linalotarajiwa kujengwa.

Ni jukumu la mhandisi huyu kuandaa michoro ya uimara wa jengo kwa maana ya namna nondo na zege na hata vyuma vingine vitakavyokuwa na ukubwa wake kwa maeneo kama nguzo (column), msingi (foundation) bimu (beams), kuta, ngazi za ghorofa na slabu (slabs) kwa upande wa majumba. Halikadhalika huandaa michoro kwa ajili ya madaraja, nguzo kubwa, mabwawa n.k. 

Wakati wa ujenzi anakagua pia ubora wa bidhaa (materials) zinazotumika na namna nondo na zege zinavyotengenezwa kama vinafikia ubora unaotakiwa kama alivyobuni kimahesabu.

Inapotokea jengo limeanguka kwasababu zisizotokana na nguvu za asili kama mtetemeko ya ardhi na milipuko ya bomu kwa mfano, mhandisi ndiye hupewa majukumu ya kuchunguza sababu za kihandisi zilizopelekea hitilafu iliyosabababisha jengo kuanguka kama iivyotokea maeneo ya Kisutu Jijini Dar es Salaam miaka michache iliyopita. 

Mkadiriaji Majenzi/Quantity Surveyor(QS)
Mkadiriaji majenzi kwa baadhi ya nchi hutambulika kama Cost Engineer. Ni sawa na kusema ndiye mhasibu kwenye sekta ya ujenzi. 

Majukumu makubwa ya mkadiriaji majenzi ni kufanya makadirio ya gharama za mradi wa ujenzi. Makadirio hufanyika wakati wa kubuni wazo la mradi, wakati wa ujenzi na wakati wa kuandaa mkataba wa ujenzi kwa ajili ya kupatana na mkandarasi. Makadirio haya hufanyika kimahesabu kwa majengo mapya au yanayokarabatiwa ama kuboreshwa. 

Mkadiriaji majenzi hufanya kazi katika sekta zote mpaka kwenye uchimbaji madini, miundombinu, na majengo ya nyumba za kuishi na majengo makubwa ya viwanda na taasisi za umma au jumuia. Ili kuweza kukamilisha kazi yake hulazimika kutafuta kiasi (quantity) cha visaidizi kama nguvu kazi, zana za kazi, bidhaa za ujenzi n.k. 

Katika miradi mkubwa ya ujenzi QS ndiye huwajibika kufanya yafuatayo
a. Kufanya makadirio ya bajeti ya mradi
b. Kuchanganua madhara yanayoweza kujitokeza kwa kubadilisha dizaini ya jengo na bajeti yako
c. Kuandaa BOQ (kitabu cha makadirio ya gharama na kiwango cha kazi) ambayo husaidia wakati wa kumtafuta mkandarasi wa kutekeleza ujenzi
d. Kuandaa kamabrasha ya tenda za ujenzi na kusimamia zoezi zima
e. Kuhakiki kazi ya ujenzi iliyofanyika na kuipa thamani yake kwa ajili ya kuruhusu malipo kufanyika kwa mkandarasi kwa kiwango cha kazi alichofanya.
f. Kusimamia mabadiliko yate ya kimuundo na kiujenzi na hata gharama wakati ujenzi unaendelea tofauti na kilichobuniwa awali.
g. Kuandaa hesabu za malipo ya mwisho kwa makandarasi ilikwa mmradi umekamilika kwa namna taratibu na sharia za ujenzi zinavyoelekeza na majukumu mengine. 

Mjenzi/Builder
Mjenzi au builder husoma na kuielewa michoro yote na maelekezo mengine na kuangalia inaoana vipi. Anachanganua uwezekano wa jengo kujengeka na namna litakavyotunzika kama lilivyobuniwa. Ni sawa na kusema huyu ni mhakiki ingawa kwa hapa kwetu ni nadra kuwakuta wataalamu hawa kwa majukumu haya kama mtaalamu wa pembeni. Mara nyingi wanakuwa kama sehemu ya wakandarasi.

Mhandisi wa Huduma za Jengo/(Building Service Engineer)
Kwa kawaida jengo halikamiliki kwa kuwa na ubunifu wa jengo lenyewe tu na uimara wake. Kwasababu kila jengo ni maalumu kwa matumizi Fulani huwa kunakuwa na huduma muhimu za kuwawezesha watumiaji wa jengo hilo kuweza kulitumia. Huduma tunazozizungumzia hapa ni kama mfumo wa maji safi na machafu, mfumo wa umeme, mfumo wa mawasiliano ya kitekinohama nausalama.

Huduma nyingine ni mfumo wa kukabiliana na hitilafu ya moto, mfumo wa usafirishaji kwenda na kutoka ghorofani (vertical transportation) na mfumo wa kuweka hali ya ujoto au baridi na kutoa hewa chafu nje ya jengo (mechanical ventilation)

Huduma zote hizi hubuniwa na kusimamiwa na mtaalamu anayetambulika kama Mhandisi wa Huduma za Jengo (Services Engineer) akifanya kazi kwa ushirikiano wa karibu na wataalamu wengine ambao nimeshawaelezea hapo awali. 



Mafundi au Artisans
Hawa ndio watu wanaofanya kazi kwa vitendo eneo la ujenzi wakiwa na ujuzi wa namna tofauti tofauti. Mafundi mchundo (Technicians) wanaingia kundi hili pia wakiwa na utaalamu (skills) kwa maeneo tofauti tofauti ya ujenzi kama ufundi seremala, ufundi chuma, ufundi tope (masonry) n.k. 

Wataalamu Washauri (The Consultants)
Kila mradi uliofuata taratibu za ujenzi kwa mujibu wa sharia zetu unalazimika kuwa na timu ya washauri wataalamu kwa msingi kwamba mmiliki (Client) anayetaka kufanya maradi wa ujenzi anaweza kuwa sio mtaalamu wa maswala ya ujenzi na hata akama atakuwa na utaalamu hataweza kuwa na uelewa wa kila kitu. Hivyo inamlazimu kuwa na timu ya watu watakaomshauri na kumsaidia kufanikisha mradi wake ili aweze kupata thamani halisi ya alichowekeza na kilichojengwa kama vinawiana. 

Wataalamu Washauri ni mjumuiko wa wataalamu wote niliowaeleza hapo mwanzo, wataalamu kama Mbunifu Majengo, Mkadiriaji majenzi, Wahandisi wa jengo na Huduma, na wataalamu wengine. 

Hawa washauri wanatakiwa kushirikishwa kuanzia mwanzo kabisa wazo la mradi linapoanza kwsasababu kimajukumu washauri hawa ndio huchukua nafasi ya mmiliki au tajiri wa mradi na kumuwakilisha katika maswala ya kitaalamu. 

Mkandarasi/Building Contractor
Mkandarasi kwa lugha rahisi anahesabika kuwa ni mkusanyiko wa timu ya wajuzi wa masuala ya ujanzi pamoja ambao wao majukumu makubwa ni kubadilisha michoro na kuifanya kuwa uhalisia wa kilichobuniwa. Mkandarasi huwajibika kukusanya vifaa na bidhaa za ujenzi na kutumia utaalamu wa watu wake kufanikisha ujenzi husika mpaka kukamilika kwake na kuwa tayari kwa matumizi yaliyokusudiwa. Kawaida katika miradi mingi kunakuwa na Mkandarasi mkuu na wakandarasi wadogo ambao kwa magawanyo wa majukumu wao hufanya shughuli nyingine ambazo wengine hawawezi. Ndio haswa wanaohusika na ufanikishaji wa huduma za jengo kama nilivyozifafanua awali.

Mkandarasi ninayemzungumzia hapa kisheria ni yule ambaye amepata leseni ya kufanya kazi kutoka Bodi ya Makandarasi nchini (Contractors Registration Board).

Mpaka kufikia hapa ni matumaini yangu kuwa kwa kiasi Fulani nimeweza kudadavua maswala machache muhimu ambayo kimsingi yanatoa jibu la tunakosa nini tusipotumia wataalamu kwenye ujenzi wa nyumba zetu. Kama umebahatika kupeleleza nyumba zilizojengwa kwa kushirikisha wataalamu hata kwa hatua mojawapo na zile ambazo zimejengwa bila kuwashirikisha utakubaliana name kuwa zilizoshirikisha wataalamu zinaubora na umaridadi mzuri tofauti na zile ambazo hazikuhusisha wataalamu hata kwa ushauri tu. 

Tukutane tena katika sehemu ya mwisho ya mfululizo wa makala hii ambapo tutaweza kufahamu sasa nini tunachokikosa. 


Mwandishi/Mchambuzi
Tumainiel W. Seria
BSc. Building Economics (Hons), UCLAS
GQS (Registered with AQRB)
Director: S&L CostCare and Planners
P.O Box 16094 Arusha
+255757718080
seria.tw@gmail.com

No comments: